Taasisi zinazotetekeleza programu ya AFDP zatakiwa kufanya kazi kwa malengo
Na; Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge na Uratibu, Jenista Mhagama amezitaka taasisi zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kufanya kazi kwa malengo na kwa wakati ili kutekeleza mpango kazi ambao umewekwa katika programu hiyo. Kauli hiyo ameitoa leo Alhamisi Julai 27, 2023, alipokuwa katika […]
Na; Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge na Uratibu, Jenista Mhagama amezitaka taasisi zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kufanya kazi kwa malengo na kwa wakati ili kutekeleza mpango kazi ambao umewekwa katika programu hiyo.
Kauli hiyo ameitoa leo Alhamisi Julai 27, 2023, alipokuwa katika ziara ya kikazi ya kutembelea Shirika la Uvuvi la Nchini (TAFICO) jijini Dar es Salaam, ambapo amesema (TAFICO) ni moja ya taasisi za Serikali iliyopewa majukumu katika programu ya kuendeleza Kilimo na Uvuvi, yenye lengo kubwa la kuongeza tija na faida katika mazao yatokanayo na kilimo na uvuvi ikiwa ni pamoja na ukuzaji wa mazao yatokanayo na viumbe maji kupitia teknolojia ya kisasa.
Akizitaja Wizara na Tasisi zinazotekeleza Programu hizo chini ya Uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu kuwa ni Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Uchumi wa Buluu na Uvuvi Zanzibar, (TAFICO) na (ZAFICO).
Waziri Mhagama amezitaka taasisi hizo kuzingatia ubora na thamani ya fedha katika mradi mzima: “Natarajia kila senti itakayowekezwa katika mradi huu itaenda kujibu na kuleta matokeo halisi tena yakiwa chanya na yatakayosaidia nchi yetu kusonga mbele na kupata maendeleo endelevu kwa wananchi na taifa kwa ujumla,” amesema Mhagama.
Awali, akizungumza katika ziara hiyo, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu, Dk. Jim Yonazi alisema, Serikali imeweka mkazo katika kuhakikisha kwamba nchi inanufaika na rasilimali maji hasa katika eneo la uvuvi, kupitia mradi wa (AFDP).
“Sisi kama watendaji tupo tayari kuweka msisitizo na kuhahakisha kwamba haya yote yanakamilika kwa wakati na kuleta tija kwa taifa letu,” alisisitiza Dk. Yonazi.
Kwa Upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika hilo,Dennis Simba alisema kuwa, (TAFICO) imejipanga na ipo tayari katika kuhakikisha kwamba inafungua njia ya kwenda katika uvuvi wa Bahari kuu na mnyororo mzima wa thamani, na kuongeza kuwa miradi 11 iliyopo katika programu hiyo itatekelezwa kwa wakati na kwani Serikali imeonesha nia ya dhati ya kufungua uchumi wa Bluu.
Awali, Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Bodi ya (TAFICO), Dk. Eliamini Kasembe, alisema Serikali ya Awamu ya Sita imeamua kufufua shirika hilo kwani lina manufaa makubwa kwa wananchi na taifa kwa ujumla.
“Nia hii thabiti inaweza kufikia malengo ya uanzishwaji wa Shirika hili ikiwa ni pamoja na kutoa Ajira na kuchangia katika kuinua uchumi wa Taifa hili,” alisema.